SERIKALI
 ipo katika hatua za mwisho za kuilipa kampuni ya Bharti Airtel ili 
kurejesha umiliki wa asilimia 100 katika Kampuni ya Simu Tanzania, TTCL.
 
Uamuzi
 huo unaotarajiwa kutekelezwa kabla ya mwisho wa mwezi huu utaiwezesha 
TTCL kurejesha hisa zake 35% zilizonunuliwa na Airel mwaka 2001 na 
kuifanya Bharti Airtel kuwa mbia mwenza katika Kampuni hiyo. 
Waziri
 wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof Makame Mbarawa ametangaza 
uamuzi huo Jumatatu hii Mkoani Mtwara alipotembelea Ofisi za TTCL Mkoa 
wa Mtwara, kukagua mitambo na miundo mbinu ya Mkongo wa Taifa wa 
Mawasiliano.
"Serikali
 imesikia kilio cha muda mrefu cha Watanzania na wadau wote wa TTCL 
kuhusu kuondoka kwa mbia mwenza Kampuni ya Bharti Airtel. Ubia huu wa 
TTCL na Bharti Airtel utahitimishwa Rasmi kabla ya mwisho wa mwezi huu. 
"Tumefanya
 majadiliano ya kutosha, tumekubaliana kuwa Serikali iilipe Bharti 
Airtel sh bilioni 14.9 ili kurejesha hisa za 35% za TTCL na kuifanya 
Kampuni hii ya TTCL kuwa mali ya Umma kwa 100%. 
"Tutatumia
 fedha za Mapato ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ili kukamilisha 
utaratibu huu. Naiagiza Bodi na Menejimenti ya TTCL kufanya kazi kwa 
bidii na Ufanisi Mkubwa na kusimamia kikamilifu shughuki za TTCL ili 
kutimiza jukumu lake kwa Umma." Alisema Waziri Mbarawa
Kwa
 upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Prof. Tolly Mbwette amesema, 
kukamilika kwa mchakato huu ni hatua muhimu sana kwa Uhai na ufanisi wa 
TTCL na kusisitiza kuwa, mpango wa mageuzi ya kibiashara wa kampuni hiyo
 sasa utatekelezeka kwa kasi kubwa baada ya hatua hii.
Ofisa
 Mtendaji Mkuu wa TTCL, Dk. Kamugisha Kazaura amesema, jitihada kubwa za
 TTCL sasa zitaelekezwa katika kuboresha huduma kwa kutumia fedha za 
ndani na Mikopo ya wadau wa kibiashara ili kuiwezesha kampuni kuendelea 
kuwa kiongozi katika utoaji wa huduma bora na nafuu katika soko la 
Mawasiliano nchini.
Hivi karibuni, TTCL imezindua huduma za Mtandao wenye kasi zaidi wa 4G LTE na kuimarisha ubora wa huduma zake za data na sauti. 
Aidha,
 TTCL na Benki ya TIB zimeingia makubaliano ya mkopo wa fedha na dhamana
 za Benki utakaoiwezesha TTCL kupata fedha dola za Marekali milioni 329 
ili kuingiza mitambo mipya ya kisasa itakayo boresha huduma zake ikiwa 
ni pamoja na kuanzisha huduma ya miamala ya fedha kwa njia ya mtandao.

 
No comments:
Post a Comment