Uingereza
 imetoa mchango wa Shilingi Bilioni 6 kwa Serikali ya Tanzania kwa ajili
 ya kuchangia ujenzi wa miundombinu ya shule zilizopata madhara kufuatia
 tetemeko la ardhi lililotokea katika Mkoa wa Kagera tarehe 10 Septemba,
 2016.
Mchango
 wa fedha hizo umewasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
 Dkt. John Pombe Magufuli na Balozi wa Uingereza hapa nchini Mhe. Sarah 
Catherine Cooke, Ikulu Jijini Dar es Salaam muda mfupi baada ya Balozi 
huyo kuwasilisha hati zake za utambulisho.
Balozi
 Sarah Catherine Cooke amemueleza Rais Magufuli kuwa pamoja na kutoa 
mchango wa fedha hizo Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe. Theresa May anatoa 
pole kwa Serikali ya Tanzania na kwa familia zote zilizopatwa na madhara
 ya tetemeko hilo na kwamba Uingereza imeona ishirikiane na Tanzania 
katika kukabiliana na madhara hayo.
“Uingereza
 imeguswa sana na maafa yaliyowakumba wananchi kufuatia tetemeko 
lililotokea Kagera, tunapenda kuona wananchi wanasaidiwa na wanafunzi 
wanaendelea na masomo” amesema Balozi Sarah Catherine Cooke.
Kwa
 Upande wake Rais Magufuli amemshukuru Waziri Mkuu wa Uingereza kwa 
mchango huo ambao utasaidia juhudi za Serikali za kuhakikisha inarejesha
 miundombinu iliyoharibika zikiwemo shule.
“Mhe.
 Balozi Sarah Catherine Cooke naomba unifikishie shukrani zangu za dhati
 kwa Waziri Mkuu wa Uingereza Mhe. Theresa May na umueleze kuwa kwa 
niaba ya watanzania hususani waliopatwa na madhara ya tetemeko la ardhi 
tumeguswa sana na moyo wake wa upendo kwetu” amesema Rais Magufuli.
Rais
 Magufuli na Balozi Sarah Catherine Cooke pia wamezungumzia uhusiano na 
ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Uingereza ambapo Rais 
Magufuli ametoa wito kwa Balozi huyo kuendelea kuwahamasisha 
wafanyabiashara na wawekezaji wa Uingereza kuongeza uwekezaji wao hapa 
nchini na kwamba Tanzania itaendeleza na kukuza uhusiano huo.
“Uingereza
 ni rafiki na ndugu wa kweli na wa kihistoria kwa Tanzania, tunatambua 
kuwa nchi yenu ni mdau mkubwa na muhimu wa maendeleo yetu, hivyo 
tusingependa kupoteza rafiki na ndugu yetu, tuendelee kushirikiana kwa 
manufaa ya wananchi.
“Natambua kuwa Uingereza ina utaalamu mkubwa katika masuala ya gesi hivyo nawakaribisha waje wawekeze katika sekta ya gesi” amesisitiza Rais Magufuli.
Aidha,
 Rais Magufuli amesema Serikali itahakikisha fedha zote zinazotolewa kwa
 ajili ya kusaidia kukabiliana na madhara ya maafa ya tetemeko la ardhi 
lililotokea mkoani Kagera zinafikishwa kwa walengwa na ameonya kuwa 
watakaothubutu kuiba fedha hizo watashughulikiwa.
Dkt.
 Magufuli amebainisha kuwa baada ya kutengua uteuzi na kuchukua hatua 
nyingine dhidi ya aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Bw. Amantius
 Msole na Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba Bw. Steven Makonda pamoja na 
kumsimamisha kazi Mhasibu Mkuu wa Mkoa wa Kagera Bw. Simbaufoo Swai, 
amemtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Dkt. Charles Kimei 
awachukulie hatua watumishi wa Benki hiyo walioshirikiana na watumishi 
hao kufanya njama za kuanzisha akaunti nyingine ya benki yenye jina 
linalofanana na akaunti rasmi ya “Kamati ya Maafa Kagera” kwa lengo la 
kujipatia fedha”
Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
28 Septemba, 2016

 
No comments:
Post a Comment